Maziwa, mito bahari na chemchemi lukuki,
Nchi iliyo tajiri, lakini haizinduki,
Akili zakifakiri, ndizo zinazotamalaki,
Wasiojisaidia, Mola hawasaidii!
Ardhi yake bahari, nini hakistawiki?
Siasa za kikafiri, dhuluma zinahakiki,
Mkulima hanawiri, anyonywa mpaka haki,
Wasiojisaidia, Mola hawasaidii!
Wazee na matajiri, nchi wanaimiliki,
Ni heri nusu ya shari, kwao hilo hawaafiki,
Haijai bilauri, njaa yao haishibiki,
Wasiojisaidia, Mola hawasaidii!
Kiu yao ya tanuri, katu haimaliziki,
Ukubwa wao jeuri, na kazi haifanyiki,
Watakacho ufahari, wala si mikiki mikiki,
Wasiojisaidia, Mola hawasaidii!
Madini yamedhihiri, raia hanufaiki,
Akili zatahayari, uongozi kuafiki,
Ni nani mwenye habari, ambazo haziandikiki,
Wasiojisaidia, Mola hawasaidii!
Na misitu kwa ekari, mbao bei haishikiki,
Makazi yatuadhiri, watu hawathaminiki,
Wakubwa waona fahari, nje kwenda kuhakiki,
Wasiojisaidia, Mola hawasaidii!
Ndani hamna safari, ila zile za falaki,
Zanyong'onyea suduri, uhai hautamaniki,
Na walio na kiburi, hili halikubaliki,
Wasiojisaidia, Mola hawasaidii!
Viwanda tumeghairi, tunawapa mamluki,
Uzalishaji johari, bilavyo hatujengeki,
Viongozi washairi, na tungo hazighaniki,
Wasiojisaidia, Mola hawasaidii!
Kuwaomba matajiri, hulka siiafiki,
Twajidhalilisha ari, hamsini hatuamki,
Tuutazame urari, tutumie wetu mkuki,
Wasiojisaidia, Mola hawasaidii!
Vijana wanasubiri, na akili wastahiki,
Mapinduzi kuabiri, kama nchi haijengeki,
Na huu si ujibari, nia tutaiafiki,
Wasiojisaidia, Mola hawasaidii!
Saturday, October 15, 2011
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment