Friday, July 3, 2009

Furaha yangu

1.
Furaha yangu mwenzangu, nawe kushirikiana,
Niwe wako uwe wangu, si usiku si mchana,
Mzigo wako ni wangu, tutakujapokezana,
Siue furaha yangu, kuniacha peke yangu.

2.
Furaha yangu daima, mimi na wewe kuteta,
Waziwazi kuyasema, ya furaha na kujuta,
Maovu pia na mema, kuyamwaga na kuchota,
Siue furaha yangu, kuniacha peke yangu.

3.
Furaha yangu pekee, niwe lako kimbilio,
Itokeapo ujikwae, mbiombio kwangu njoo,
Usijali niegemee, uchechemeapo leo,
Siue furaha yangu, kuniacha peke yangu.

4.
Furaha yangu 'kilia, nifute machozi yako,
Kwa hariri kitambaa, utulie wajihi wako,
Kisha nitakupepea, zirudi pumzi zako,
Siue furaha yangu, kuniacha peke yangu.

5.
Furaha yangu ujue, sisi kama wana pacha,
Nataka ulitambue, wewe si wa kuniacha,
Ni ubavu uning'oe, kweli hai utaniacha ?
Siue furaha yangu, kuniacha peke yangu.

6.
Jasho lako marashi, langu kwako Jasmini,
Bashasha yako nakishi, Utani wangu afueni,
Tomasa yako ucheshi, Papasa yangu hisani,
Siue furaha yangu, kuniacha peke yangu.

7.
Ukichoka kiti chako,kitakachokubembeleza,
Pale ukasirikako, hasira nitaimaliza,
Huko uhangaiko, mie nitakupumzisha,
Siue furaha yangu, Kuniacha peke yangu.

8.
Njoo tuanze chini, tupande juu pamoya,
Nipe hawa masikini, tajiri nitakufanya,
Njoo uwe yangu feni, twenzetu hadi Ulaya,
Usiue furaha yangu, Kuniacha peke yangu.

9.
Nisife na akili hizi, bila kuachia wanao,
Ukazaa na machizi, Na vichwani hamnao,
Akili kitu azizi, Chagua sana uzao,
Usiue furaha yangu, kuniacha peke yangu.

10.
Tamati ninafikia, yakini nikitegemea,
Ujumbe umekufikia, nawe yangu umeelewa,
Mikonowe imetwaa, moyoni mwangu furaha,
Nani wa kunirudishia. kama sio wewe dia ?