INAVYOELEKEA bado tatizo la umeme linaloikumba Tanzania kwa hivi sasa halijaweleka na wote, yaani, viongozi na wananchi. Katika hali kama hii ni vigumu kuona mwanga upande wa pili wa pango, hususan, kuhusiana na uwezekano wa suala hilo kupata ufumbuzi bila kuchelewa mambo yakaharibika zaidi kuliko ilivyo sasa, kisiasa na kiuchumi.
Maana tatizo letu kama nchi nyingi za Kiafrika ni lile la kushindwa kuwa na miundo na mifumo inayofanya kazi kwa sababu mbalimbali zikiwemo zile za nchi kuongozwa kwa kufuata mipango, ahadi na misaada kutoka nje. Na kushindwa kabisa kujikwanyua toka kwenye makucha ya ubepari mamboleo, matapeli wa kimataifa na mabwana wa watwana. Uongozi wowote unaojenga tabia ya ombaomba, hujenga nchi ya ombaomba. Nyumba au uongozi wowote unaojivuna na unaothamini watu wake kikwelikweli hukataa kujenga tabia ya ombaomba. Watazame ombaomba mitaani Dar es salaam na familia zao ujiulize kama watu hawa kweli wanaweza kuja kubadilika baadaye. Haiwezekani. Badala yake ,hujenga tabia ya kupenda kujitegemea, kukinaishwa na kusaidiwa na kujivunia kama wenzetu wa Korea ya Kaskazini walivyofanya kunako miaka ya 1950 pale walipotengeneza trekta lao wenyewe la kwanza na badala ya kwenda mbele, gia zote zikawa ni za rivasi tu.
Kiongozi yeyote anayewadharau raia wake: kwa kuwaita wavivu, wezi, wategaji, wababaishaji atambue sio raia wake wenye tatizo bali ni yeye mwenye tatizo. Kwa kifupi, mdharau chake na kuthamini wengine na vya wengine hawezi kamwe kuwa kiongozi wa kutumaniwa wala kutegemewa kuleta mabadiliko ya kimsingi katika jamii husika. China au Korea Kusini au Brazl au India au Malaysia -ingelifanya hivyo, isingekua hapo ilipo leo.
Kuwathamini kupindukia watu toka nje na kutowathmini ipasavyo raia wako mwenyewe ni mwanzo wa jengo la nchi lisilo na msingi madhubuti.
Haya ni mambo yaliyotufikisha hapa tulipo ambapo leo pamoja na kuwa na wasomi wa masuala ya umeme na nishati, hawatumiki kwa ajili hiyo, na wanaofanya maamuzi juu ya masulala hayo ni wanasiasa ambao bila shaka ni mbumbumbu katika masuala hayo na uelewa wao unategemea maelezo wanayopata kutoka kwa wanaojua wanachokizungumza.
Aidha, kutokana na hayo hapo juu imekuwa vigumu kwetu kupambanua kati ya yale ambayo tunatakiwa tuyafanye sisi wenyewe ima-fa-ima na yale ambayo kwa sababu fulani fulani tunalazimika kuomba msaada au ushirikiano toka kwa wengine.
Hakuna asiyetambua kwamba, ili tuendelee nchi yetu inahitaji : chakula, maji; hewa safi; mazinigira salama; afya bora na usalama kwa watu wetu; umeme au nishati mbadala; reli ya kisasa; barabara zinazopitika bila usumbufu wakati wote; makazi bora kwa watu; usafiri wa anga na majini; masoko yanayofikika ndani na nje ya nchi; ushauri mzuri kwa waliotutangulia; utafiti na kuyaelezea kwa urahisi masuala mbalimbali ili yaeleweke na wengi nchini na elimu inayosaidia kutatua matatizo yetu au kutumia fursa za maendeleo zilizopo ndani ya mipaka yetu na nje ya mipaka yetu.
Tujihusishe na hili suala la umeme tu na hayo mengine tuyaache hadi wakati mwingine. Inshallah. Kuna vitu ambavyo 'piga-ua' ni lazima Watanzania waiunde au watengeneze wao wenyewe kwa kutumia watu wetu waliosoma na wasiosoma ili mradi ni wabunifu, watundu na wanaoweza kujaribu bila kukatishwa tamaa na kushindwa katika maisha yao yote. Hata wakishindwa mara ngapi! Na mimi siamini kama tukiwatumia wasomi wetu, wataalamu wetu, mameneja wetu, wanajeshi wetu na vijana wetu kikamilifu tuna sababu ya kushindwa zaidi ya mara mbili tatu tu! Tunashindwa kwa sababu hatuwatumii watu wetu ipasavyo! Tunashindwa kwa sababu wanasiasa wetu wamejifanya pia wao ndio wataalamu na magwiji wa uchumi na maendeleo ya jamii.
Lakini kama tutawatumia maprofesa wetu wa vyuo vikuu na wanafunzi wao katika taaluma ya umeme na nishati sio tu tunaweza kupata ufumbuzi wa muda mfupi bali wa kudumu wa matatizo yetu.
Ni kitu cha kuhuzunisha kuwa pengine kutokana na viongozi wetu wa vyuo vikuu kujikita zaidi kwenye siasa badala ya uchumi na uzalishaji mali, mahala kama Chuo Kikuu cha Dar es salaam, chenye idara ya Uhandisi wa umeme hakina mifano yoyote inayofanya kazi kama vile mashamba ya upepo wa umeme au ya solar energy au uzalishaji umeme kwa njia nyingine mikoani - na inayoweza kulipiwa na kufadhalilwa na kupanuliwa kukidhi mahitaji yetu ya umeme.
Msiba mmoja mkubwa kwa taifa letu ni lile la kuwa na elimu na wasomi wanaojengwa ili na wao kutegemea vitu na mitambo inayozalishwa nje kwa maendeleo ya watu na nchi yetu.
Ni kwa njia hii tu ndiyo tutaweza kupata maendeleo ya kweli, ya kudumu na endelevu na sio kwa kutegemea kila kitu kitoke kwa wengine.
Vitu hivyo ni pamoja na mashine na mitambo kwa ajili ya uzalishaji umeme; utekaji, uvutaji na usmbazaji na umwagiliaji maji; uchimbaji madini; ujenzi wa bandari; ujenzi wa reli; ujenzi wa viwanja vya ndege; ujenzi wa barabara; ujenzi wa madaraja; miundombinu ya mawasiliano; na zana au vifaa mbalimbali vinavyohitajika katika ujenzi wa majengo na makazi katika nchi.
Msingi wa nchi yoyote usipoanzia katika mambo hayo hapo juu, nchi haiwezi kamwe kuuacha umaskini, achilia kuwa na maendeleo endelevu. Mpango na mkakati wowote unaoshindwa kuibua mambo haya, kisha kuyatafakari, kuyainisha na kuyapa kipaumbele katika maendeleo ya nchi ni mpango au mkakati unaofaa kutupwa jalalani pindi unapogundulika kwamba upo na unagharamiwa na kodi za wananchi. Ni mpango unaoihukumu nchi kubaki kwenye makucha ya wakoloni, mabepari na mabeberu kwa faida zao na wala sio kwa faida ya nchi na watu wake. Ni mapango unaowalazimisha watu wa nchi fulani wawe ombaomba, huku rasilimali za nchi zikichotwa kwenda kuwafanya watoa sadaka matajiri na matajiri zaidi. Ni mpango na mkakati unaomfanya raia wa nchi hii kuwa mtumwa wa wakoloni wa zamani na vibarakala wao na utandawazi na mumiani wake.
Kwa maneno mengine matatizo yetu mengi, likiwemo hilo la umeme ni matatizo yanayoweza kupatiwa ufumbuzi wa haraka na kudumu kwa kutumia vyema rasilimali watu yetu na rasimali watu toka nje pamoja na matumizi sahihi ya rasilimali zetu nyingine.
Hili linaweza kufaulu tu katika nchi ambayo haijvunii na haiwalindi mafisadi kama sehemu ya uongozi wake; inayotambua maendeleo yetu kama rasilimali zetu zinatumika vizuri, yanaweza kugharamiwa na watakaopata ujuzi na uzoefu katika mipango yetu mbalimbali ya maendeleo nchini, wakati watakapokwenda kuwafanyia Waafrika wengine kazi kama hii. Fisadi wa Kitanzania, ni mwizi anayejiibia shati lake mwenyewe. Fisadi wa kimataifa, haibi cha ndani, hukwapua cha nje kuja kuwafaa wenzake walio nyumbani na sio vinginevyo. Na uwezo wa kutajirika kwa kutumia rasilimali za wengine, ikiwa ni pamoja na umeme, kutokana na nchi zinazotuzunguka Watanzania tunao, isipokuwa hatuna uongozi unaoona wala kuelewa hili.
Vilevile, hili huweza kufanyika tu katika nchi ambayo chama tawala hakiendeshi nchi kana kwamba ni wabunge wake tu na wanachama wake wenye uwezo wa kuwa mawaziri, wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya, makatibu wakuu, wakurugenzi, mamaneja, majaji, mabalozi na wafanyakazi nchi za nje na wasimamizi wa taasisi mbalimbali. Bali kinaendesha nchi kwa kutumia akili, uwezo na michango ya Watanzania wote bila kujali ni wafuasi wa chama tawala au la.
Miaka hamsini baada ya Uhuru dunia imeipa fursa kubwa nchi yetu ya kuchagua na kuwakaribisha wataalamu tofauti toka sehemu mbalimbali duniani wenye ujuzi na uzoefu wa kila aina kuanzia watengnenezaji baiskeli hadi waunda satelaiti na roketi. Hawa ni binadamu wenzetu amabo leo ni 'jobless' pamoja na utaalamu au elimu na uzoefu wao, walioko huko Marekani, Ulaya Magharibi, Ulaya Mashariki, Marekani ya Kusini na Asia. Watu ambao tukiwapatia nyumba, gari na mshahara wa kukidhi mahitaji yao ya msingi wapo tayari kuja nchini hapa kusaidiana na sisi kuifanya nchi yetu iendelee kwa kasi na haraka zaidi. Kinachotakiwa ni kutambua hili na kujipanga kulishughulikia kwa namna ambayo litakuwa ni la faida kwetu sote, kwao na sisi kadhalika. Ni rahisi, kulizungumza hili kwa maneno, lakini ukweli ni kwmba kwa uoga, uziwi na upofu wa viongozi wetu hususan kuhusiana na yale yanayoandikwa na magazeti ni GUMU KAMA GAMBA LA KOBE.
Ila kwa bahati nzuri, kutokana na kukua kwa demokrasia nchini hapa upo uwezekano kwamba hili likifumbiwa macho na watawala, haliwezi kuachwa kuokotwa na wapinzani na wanaharakati wengine wenye mapenzi ya dhati ya nchi yao na uchungu na umasikini wa wananchi wenzao.
Katika miaka hii ambayo hali ya hewa inaendelea kubadilika na hatuna ahadi wala uhakika na mvua na kwa hiyo maji yanayotiririka katika mito na mabwawa tuliyoandaa kuzalisha umeme ni makosa makubwa kuendelea kutegemea umeme wa tabaini zinazoendeshwa na maji.
Hali yetu kama nchi sasa ni afadhali ukilinganisha na Somalia. Lakini upo uwezekano mkubwa wa ukame ulioikumba nchi hii iliyo kaskazini ya Tanzania na Kenya pia kuikumba nchi yetu.
Kutokana na ukweli huu, wale wanaoshika nafasi za uongozi nchini wanapaswa kuona mbali na mbele zaidi kuliko mwananchi wa kawaida.
Tatizo letu kwa hiyo siyo tu tatizo la ukame na kukosa mvua na maji ya kuzalisha umeme bali pia ni upungufu wa mipango na mikakati ya upatikanaji nishati ya uhakika na isiyoathirika na hali ya hewa kwa kadri inavyobadilika.
Tatizo pacha ni lile la serikali kudharau na kupuuza ushauri wa watu mbalimbali kuhusiana na muundo, kazi na nafasi ya shirka la umeme la taifa (TANESCO) katika kutafuta jawabu kamili na la kuridhisha la tatizo la umeme nchini.Shirika ambalo hivi leo limebatizwa na kuitwa 'TANZANIA ELELCTRIC SUFFOCATION COMPANY'- Ni dhahiri kwamba shirika ambalo miaka 50 baada ya uhuru limeweza kuwapatia asilimia 5 tu ya Watanzania umeme halina akili wala uwezo wa kufanya makubwa zaidi ya hayo ambayo tayari limekwishayafanya. Limefikia upeo wa uwezo na ubunifu wake.
Uendeshaji wa mashirika ya umma umefanana na ule wa mzazi ambaye alimshonea mwanaye suti akiwa na miaka 10 na leo mtoto huyo ambaye ana miaka 20 eti anatakiwa kuvaa suti ileile aliyoivaa akiwa na miaka 10. Watanzania tulikuwa milioni 9 mwaka 1960. Tuliyoyafanya wakati huo hayawezi kufanywa miaka hamsini baadaye na tukiwa takriban Watanzania milioni hamsini.
Baadhi ya watu wameshawahi shirika hilo livunjwe katika sehemu nne. Uzalishaji umeme, usambazaji umeme, utengenezaji vifaa vya umeme na uunganishaji na uhudumiaji miundo-mbinu ya umeme. Na sio lazima kufanya kazi zote hizi, bali shirika/serikali iruhusu Watanzania binafsi, wanajamii na wawekezaji kuendesha shughuli hizo kwa ufanisi na ufanifu zaidi.
Wapo pia waliopendekeza kwamba kila mkoa uwe na shirika lake la umeme, badala ya kuwa na shirika la umeme la taifa, kwa kutumia rasilimali za mkoa na ubia na wawekezaji wa ndani na nje. Hawa waliamini katika falsafa ya Schumacher kwamba 'Kidogo ni kizuri na chema zaidi,' au kwa Kiingereza: 'Small is Beautiful.' Kilal mkoa ungelitafuta chanzo chake binafsi cha uzalishaji umeme bila ya kutegemea tu maji. Hili lingeliendana pia na kifungu cha katiba kinachohusiana na kuwepo na ulinganifu katika maendeleo ya taifa-kitu ambacho kimeshindikana kabisa katika sekta hii ya nishati.
Niliposikiliza mahojiano ya Mh. Jakaya Kikwete na BBC akiwa ziarani Afrika Kusini sikuweza kuacha kuona kwamba majibu yake hayakuwa yenye kuonesha imani na matumaini kwamba tatizo la umeme liko ndani ya mikono ya Watanzania . Kilichojitokeza ni kwamba ni serikali ndiyo tu iliyokuwa ikitarajiwa kulitatua tatizo hilo. Aidha, serikali ilikuwa inapaswa kulipa fedha zote za ununuzi wa mitambo ya uzalishaji umeme papo kwa hapo. Kitu ambacho sio sahihi.
Ninaamini, Watanzania wakihamasishwa kama walivyokatwa kodi na haki zao mbalimbali ili kuanzisha mashirika ya umma (yaliyokuja kubinafsishwa bila wao kulipwa chochote) wana sababu, uwezo na nia ya kuchangia kumaliza tatizo la umeme lakini kwa sharti kuwa wanakuwa nao ni wamiliki wa mashirika yatakayoanzishwa kama sehemu ya ufumbuzi wa tatizo hili.
Vilevile, watengenezaji wa mitambo ya umeme wako tayari kukodisha mitambo yao na vile vile kuuza mitambo hiyo kwa mtu kulipia kidogo kidogo hadi deni liishe.
Hata hivyo kinachoonekan hapa ni kuwa mtazamo wa ndani kwa suala hili haupo na badala yake tuna mtazamo wa nje tu. Ikiwa ni pamoja na kuamini kuwa ni lazima tupate msaada au tukope kutoka nje ili tatizo la umeme liishe hapa nchini. Au wakati mwingine, pengine ni ujanja wa kununua vikubwa vikubwa kwa gharama kubwa ili watu wapate chambele au teni pasenti yao.
Sikubaliani kabisa na wale wanaoamini kwamba tatizo la umeme limesababishwa na ufisadi na eti kuna wauza majenereta walioihona serikali ili biashara yao ya majenereta ichanganye vilivyo. Japo kuwa majenereta yanauzwa kwa fujo hivi leo, lakini adha na gharama za uendeshaji majenereta ikiwemo kwa taasisi za serikali pia, kama vile gharama za dizeli au petroli; kelele; uchafu wa mazingira; nguvu kazi ya ziada katika kuzihudumia
ni mambo yanayoitia hoja hiyo hapo juu mashakani.
Uwekezaji katika sekta hii ya umeme unawezekana kabisa kutokea ndani ya nchi. Kwa maana kwamba, kama serikali ilivyoanzisha mashirika kwa kutumia kodi za wananchi upo uwezekano wa wananchi na wawekezaji kuchangia asilimia fulani na wawekezaji wa nje wakachangia asilimia fulani. Inapendekezwa ili makampuni ya umeme yawe ni ya Watanzania basi Watanzania wamiliki asilimia 51-60 na wawekezaji toka kwingineko asilimia 40-49.
Ufumbuzi wa tatizo la umeme, hali kadhalika, utakuwa mgumu bila kufahamu mchango wa siasa katika udhairu, kudumaa na kuserereka kwa TANESCO pamoja na misaada yote ambayo shirika hili limekuwa likipata toka kwa wafadhili wa nje na malipo ya gharama kubwa za umeme kuliko nchi nyingine yoyote Afrika. Wapo wanaodai kwamba shirika hilo liligeuzwa shamba la bibi na baadhi ya wanasiasa. Kwa maneno machache, shirika hilo, halijawahi kuendeshwa kibiashara bila kuingiliwa na wanasiasa. Pamoja na mifano mingi ya uwezo mdogo wa mameneja wa Kitanzania kusimamia miradi mikubwa hazijafanyika jitihada za dhati kumpata meneja toka nje mwenye uwezo na dhati ya kutusaidia Watanzania tuondokane na tatizo hili la umeme. Netsolution, kwa kiasi kikubwa, ilikuwa ni 'dili' lililonufaisha watu binafsi na sio nchi na watu wake.
Vilevile, wanasiasa Tanzania wamejenga tabia ya kuingilia kila fani na kazi nchini na kujifanya wao ni wataalamu zaidi kuliko wataalamu wenyewe. Toka mgao huu wa umeme pamoja na kuwa na vyuo vikuu vinavyotoa shahada mbalimbali za masuala ya umeme hapajawahikuendeshwa warsha au kongamano au angalau semina yoyote iliyowashsirikisha ili michango yao kuhusu ufumbuzi wa tatizo la umeme nchini lipatikane. Hii ni kasoro kubwa sana nchi mwetu, na isipoangaliwa itatuumiza katika kila sekta na nyanja ya maendeleo kwa miaka mingi ijayo.
Kama walivyo wanafunzi wa masomo mengine, wanafunzi wa shahada za uhandisi Tanzania hawapewi fursa za kutosha kutumia elimu yao kwa utafiti na uvumbuzi kwa majibu ya matatizo yetu mbalimbali. Bajeti yetu katika kuchochea utafiti ni ndogo mno, na sidhani kuna bajeti yoyote ya kuhamasisha ubunifu na uvumbuzi nchini miongoni mwa wasomi na wasiokuwa wasomi.
Wakati vijana wa Kenya wanagundua njia mbalimbali za kuzalisha umeme ikiwemo wa kutumia magurudumu ya baiskeli, umeme kwa upepe na sasa umeme kwa chupa ya cocacola na maji, vijana wa Kitanzania wamezungushiwa kitanzi shingoni mwao kinachowatia uoga katika kuanzisha au kuunda kitu chochote kinachoweza kuwa na manufaa kwa jamii yao. Na sio suala la ujinga au kutokujua. Ni kwamba wazazi wao na serikali yao haijakaa mkao wa kudai na kupata kutoka kwa kizazi hiki kipya zaidi ya muziki wa kuiga toka Marekani au kuvaa katakei!
Kati ya vijana wasiosoma sana ni wale ambao wameshawahi kuunda redio, kompyuta, gari, ndege, helikopta, transmita za redio na kadhalika. Lakini kwa kuwa baba na mama zao sio watu wakubwa, vijana hawa wameishia kutishiwa na vyombo vya dola hadi kujenga uoga mkubwa wa kuwa wabunifu na wavumbuzi wa kitu chochote katika maisha yao yaliyobakia. Ni nani anayekosa hapa. Tanzania au mtoto anayehusika?
Hebu, chunguza wewe mwenyewe katika nchi ambayo magazeti yametoa habari za watoto au vijana waliovumbua vitu mbalimbali, je, leo hao watoto wako wapi. Wamesaidiwa au wamehujumiwa, kwa kuwa tu ni watoto wa watu wasiokuwa na uwezo?
Nchi zetu za Kiafrika zimejenga utaratibu unaowafanya wananchi waamini kwamba bila serikali matatizo yao hayawezi kutatuliwa. Serikali inaonekana kujua kila kitu,kuwa na fedha zote duniani na kuwa bila mkono au mguu wa serikali hakuna anayeweza kusogea kwenda popote. Na serikali kwa upande wake inaelekea kuamini na kudhani ndiyo peke yake yenye majibu ya matatizo yote ya kiuchumi, kijamii, kisiasa, kiutamaduni na kiteknolojia. Kitu ambacho si kweli.
Guru wa Menejimenti, Profesa Peter Drucker anasema meneja mzuri na anayefanya kazi kwelikweli, hafanyi kazi yoyote. Ndivyo ilivyo pia kwa serikali nzuri na inayofanya kazi kwelikweli. Haifanyi kazi. Tunaposema haifanyi kazi hatuna maana haifanyi chochote au inategea tu. La hasha. Meneja na serikali bora na mfano wa kuigwa hufnaya kazi kwa kupitia watu, idara na taasisi nyingine. Unapoingilia kufanya kazi za watu wengine, idara na taasisi nyingine badla aya wao kuzifanya wenyewe kuna uwezekano mkubwa wa wewe kuvuruga kazi hizo au kutokuwa na tija linganifu wala ufanifu na ufanisi. Ni vizuri viongozi na mameneja wetu walielewe hili na wajipime na kuona kama kweli wanafanya kile ambacho kiongozi au meneja anachotakiwa kukifanya na sio kufanya anayoweza kufanya karani au tarishi. Kama sio waziri au mbunge au mkuu wa mkoa kama sio mkuu wa wilaya.
Tujiulize ni nini nafasi ya jamii katika ufumbuzi wa tatizo la umeme nchini Tanzania. Hivi leo, Benki ya dunia inamwaga misaada kwa ajili ya uanzishwaji wa miradi mbalimbali ya kijamii, jambo linaloashiria uwezekano wa kushirikiana na benki hiyo kuziwezesha jamii mbalimbali kuja na mawazo na mapendekezo kuhusiana na jinsi wanajamii wenyewe wanavyoweza kuchangia katika uzalishaji umeme nchini bila ya kutegemea sana wawekezaji toka nje. Maana wawekezaji hawaji kujenga miundombinu bali kuwekeza katika biashara au uzalishaji mali kwenye eneo walilojikita. Mjenzi wa miundombinu yetu ni lazima awe Mtanzania mwenyewe, mwanajamii katika jamii husika.
Wanajamii wa maeneo mbalimbali nchini hivi leo wanasita kujiunga na shughuli yoyote inayonukia ujamaaujamaa au ushirka ushrika kwani dhana hizo zilichakachuliwa vibaya mno na viongozi waliokuwa chini ya Mwalimu Nyerere. Ni yeye tu inaelekea alikuwa na nia safi na nzuri ya kubadili maisha ya Watanzania na sio wengine, na kama walikuwepo walikuwa wachache sana na walisakamwa kupita kiasi na mafisadi na walilia ubepari wa wakati huo.
Ni vyema pia kuzijua njia mbalimbali za kuzalisha umeme. Kisha kuainisha ni ipi au zipi ambazo zinaweza katika muda mfupi kutupa nafuu katika tatizo hili na zile ambazo zinahitaji muda na uwekezaji mkubwa zaidi.
Ziko njia mbalimbali za kuzalsha umeme zinazojulikana kufikia sasa. Njia hizo ni pamoja na mchakato wa nyuklia; samadi na takataka mbalimbali; mvuke; mashamba ya umeme wa solar; mashamba ya umeme wa upepo; mafuta ya petroli au dizeli na maji.
Tanzania inasemekana haijafikia hali ya kujitosheleza kiuwezo na kiusalama kuzalisha umeme kwa mchakato wa uranium ijapo tumejaliwa madini hayo. Kwa hiyo, hii sio njia ya kutusaidia katika siku za karibu.
Umeme kwa maji ndio huo ambao unatuongezea umaskini, maafa na dhiki zisizokweisha.
Nao huu unaweza kurudia hali yake ya kawaida endapo mipango yetu ya uoteshai miti, utunzaji mazingira na vilivyomo na hususan kwenye maeneo ya vyanzo vya maji milimani au chini ardhini itafanikishwa.
Uzalishaji umeme kwa kutumia samadi na takataka mbalimbali; upepo; mafuta ya petroli au dizeli ndio njia zinazoweza kuchangia haraka zaidi kumaliza tatizo hili.
Kwa jiji kama Dar es salaam uzalishaji umeme kwa kutumia takataka ni kitu kinachowezekana. Na njia hii itaua ndege wawili kwa jiwe moja. Kwanza, utaongeza megawati za umeme kwenye mtandoa wa umeme na pili utafanya jiji hili kuwa safi daima.
Mashamba ya umeme wa solar na upepo kwenye mikoa yenye jua na upepo wa kutosha yanaweza kuchangia gridi ya taifa kwa megawati kadhaa.
Kwenye miji na wilaya ambazo zina upepo wa kutosha ni dhahiri tukishirikiana na nchi kama Denmark na Netherlands tunaweza kupata 'shortcut' za kupata mitambo na vifaa vinavyohitaji na kuzalisha umeme chini ya mwaka mmoja.
Umeme wa jenereta zinazotuchafulia hali ya hewa, mazingira na kutupigia makelele unastahili kudhibitiwa na kuvumuliwa tu kutokana na ukweli kuwa hakuna ujanja mwingine.
Mitaani ili tusichafue zaidi hali ya hewa ni vyema maduka au makampuni kadhaa yakaungana na kununua jenereta kubwa zinazoweza kutosheleza maduka au makampuni yote yaliyo sehemu hiyo badala ya kila mmoja kuwa na kijenereta chake na hivyo kusababisha uchafuzi mkubwa wa mazingira kwa moshi, kelele na hewa ya carbon monoxide.
Inafaa pia kuuliza kama nchi zilizotuzunguka, yaani, Msumbiji, Malawi, Zambia, Kongo Kinshasa, Rwanda (ambayo imefanya kazi nzuri sana katika upatikanaji umeme kwa watu wake), Burundi, Uganda na Kenya zina hali gani kiumeme na tunaweza kushirikiana nazo vipi ili tuzalishe umeme kwa pamoja utakaotusaidia sote kupunguza au kumaliza kabisa tatizo letu la umeme.
Sunday, July 24, 2011
Subscribe to:
Posts (Atom)
