Ukitanguliza mwili,
Nyuma ifate akili,
Hupati pendo la kweli,
Na roho hugawanyika!
Siukimbilii mwili,
Najua wake muhali,
Umkutapo baradhuli,
Pendo sumu hugeuka.
Naitafuta akili,
Tena kwa hali na mali,
Sio kwayo taamuli,
Bali kwayo tajamali.
Naitafuta kauli,
Murua tena sahili,
Itoayo afadhali,
Mashaka yanaponifika.
Nazitafuta dalili,
Za bashasha na adili,
Na pendo bila ubahili,
Nikatakwa, nikataka.
Nazitafuta amali,
Za majibu na maswali,
Kuzijenga zetu hali,
Toka chini, juu tukafika.
Naitafuta asali,
Toka nyuki wa asili,
Na sio ile ya kunakili,
Nilambe na kutosheka!
Sitaki nafuu ghali,
Nikajabwagwa chali,
Bila kisomo cha Laili,
Nyota njema ikishuka.
Sitaki cha bilkuli,
Ima fa ima kivuli,
Cha mshaka ya samli,
Kupika kisichopikika.
Sitaki kiwiliwili,
Nataka yako akili,
Inifanye mie kamili,
Kiroho pia kimwili!
Tuesday, June 30, 2009
Harufu ya Jasmini
Linasifiwa waridi, tena sana duniani,
Nani hili kulikaidi, asiyelisifu nani?
Ni wachache kwa idadi,waridi wasothamini,
Mfano mie kusifu, harufu ya Jasmini.
Kulienzi sina budi,waridi rangize shani,
Hautimii mradi, kutosifu Jasmini,
Kwalo mimi shahidi, kwa macho na moyoni,
Nd'o kisa mie kusifu, ua lake Jasmini!
Ua hili maridadi, kalijalia Manani,
Linatia ubaridi, joto ukilibaini,
Na lapandisha mdadi, baridi ikikuhaini,
Hakika yanipendeza, harufu ya Jasmini.
Sio wengi hulifaidi, linapenda faraghani,
Mchana katu abadi, harufuye huioni,
Ila usiku taradadi, nje, uani na chumbani,
Utaisikia kokoe, harufu ya Jasmini.
Chumbani bure waridi, ni ndogo yake thamani,
Kitandani hufaidi, ila uwe na Jasmini,
Huba huwa kama Iddi, sikuzote u rahani,
Usingizi laini kwa harufu ya Jasmini!
Nani hili kulikaidi, asiyelisifu nani?
Ni wachache kwa idadi,waridi wasothamini,
Mfano mie kusifu, harufu ya Jasmini.
Kulienzi sina budi,waridi rangize shani,
Hautimii mradi, kutosifu Jasmini,
Kwalo mimi shahidi, kwa macho na moyoni,
Nd'o kisa mie kusifu, ua lake Jasmini!
Ua hili maridadi, kalijalia Manani,
Linatia ubaridi, joto ukilibaini,
Na lapandisha mdadi, baridi ikikuhaini,
Hakika yanipendeza, harufu ya Jasmini.
Sio wengi hulifaidi, linapenda faraghani,
Mchana katu abadi, harufuye huioni,
Ila usiku taradadi, nje, uani na chumbani,
Utaisikia kokoe, harufu ya Jasmini.
Chumbani bure waridi, ni ndogo yake thamani,
Kitandani hufaidi, ila uwe na Jasmini,
Huba huwa kama Iddi, sikuzote u rahani,
Usingizi laini kwa harufu ya Jasmini!
Subscribe to:
Posts (Atom)
