VIONGOZI wa Tanzania toka chini hadi juu wanakiri kwamba makosa yalifanyika katika kukaribisha wawekezaji katika uchimbaji madini nchini na inaelekea kitu kama hicho pia kinatokea katika shughuli za uchimbaji madini.
Makosa hayo ni pamoja na kufanya maisha na makazi ya wazawa wa maeneo husika kama vile hayana thamani kabisa; hawana urithi katika eneo husika wa madini na mali asili yake; kuwa serikali kuu ndiyo yenye sauti ya mwisho kuhusu maeneo ya wakazi na wenyeji husika; kwamba kuna watu waliopewa chochote kwa jina lolote lile ili kupata mikataba ambayo inawaruhusu kuchimba na kuchukua madini yetu sawa na bure; na kwamba baada ya Watanzania kuwa masikini kwa zaidi ya karibia miaka hamsini toka wawe huru; uwekezaji na ubinafsishaji huu kwa wageni ni hakikisho rasmi kwamba wataendelea kuwa masikini kwa miaka hamsini zaidi ijayo kama sio miaka 100 na zaidi.
Hata hivyo, wahusika wakuu ikiwemo kampuni moja maarufu na yenye jina kubwa duniani na iliyo na mirija katika makontinenti na nchi kadhaa ni kampuni iliyojenga sifa ya kuwatumia viongozi mbumbumbu, waroho na wasio na uchungu na watu wao na maendeleo yao ili kuwekeza kwenye nchi hizo na kuendeleza himaya na utajiri wake katika migodi, uchimabaji na uuzaji madini wakati mwingine katika nafasi ya ukiritmba na faida za kutisha.
Tanzania chini ya uongozi ulioridhika, kutoshekana na unaoamini kwamba Watanzania wengi wanaishi kwa zaidi ya miaka 1,000 hawana haraka kabisa na kulitazama upya jambo hili na kuchukua hatua mwafaka kwa wakati mwafaka. Na hili linafanyika wakati kuna ripoti zisizokanushika kwamba kuna mamia kama sio maelfu ya binadamu na wanyama katika maeneo fulani wanadhurika na wengine hata kufa kutokana na uchimbaji madini wa kampuni hii na nyingine kama hizo ambao zimepewa migodi kama zawadi na viongozi wetu.
Wakati tunaadhimisha miaka 12 ya kifo cha Baba wa Taifa ni wakati mzuri kutafakari kwanini mzee hakuwa na haraka na shughuli za uchimbaji madini. Na kwanini alikuwa mstari wa mbele kuanzisha Kitivo cha Jeolojia pale Mlimani na kisha kuhamasisha nchi zingine za Afrika Mashariki ili Tanzania iwe kituo kikuu cha utafiti wa madini Afrika Mashariki na kati. Juhudi ambazo kwa sababu moja au nyingine zimekwamishwa mahala fulani na leo tunaambiwa eti sababu moja ya kuruhusu uwekezaji sawa na bure eti ni kwa sababu hatuna vifaa wala wataalamu wanaoweza kutuwezesha sisi wenyewe kuchimba madini yetu. Jambo kama hili sio tu ni vigumu kueleweka na kuaminika bali linaonyesha kwamba tuliowapa kazi ya uongozi hawaongozi bali wanacheza na nchi na maisha yetu kutokana na sababu wanazozijua wao wenyewe.
Hata hivyo, nchi za Argentina, Bolivia, Ecuador na Peru zinatuonesha kwamba wananchi wanaweza kuikataa mikataba dhalimu iliyopitishwa kisiri na kiwiziwizi na walioko madarakani na kudai mikataba mipya itakayokuwa na manufaa na maslahi kwa wazawa wa maeneo husika na nchi nzima kwa ujumla.
Kwa wale waliotazama hali ilivyokuwa huko Argentina na jinsi Waargentina walivyosimama kidedea na kuifosi Barricks kubadili mikataba yake ya kidhalimu (Al Jazeera, Oktoba 14, 2011) atakuwa bila shaka amefaidika kwa mengi ikiwemo hatua kikundi cha kijamii kinachohitaji kupitia ili kuhakikisha mapinduzi haya ya kukabili makampuni ya kimataifa yenye tabia za kitapeli na kidhalimu kutokana na kuwatumia viongozi wenye ubinafsi na wanaojali maslahi ya kikundi kimoja katika nchi na wasioona mbali na mbele kwenye nchi masikini kama Tanzania.
Ingawa mikataba ya kuuza au kukodisha migodi kwa wageni imeshasainiwa na wageni wanaendelea kufaidika na dhahabu na madini yetu mengine bado hatujachelewa kabisa kuibadili hali hii. Tunaweza sisi wananchi, tukisaidiwa na wanasheria wetu na vyama vya siasa vyenye viongozi wenye uchungu na dhiki na umaskini wa Watanzania kuidhibiti hali hii na fumba na kufumbua tukajikuta tuna uchimbaji madini nchi wenye manufaa na tija kwa Watanzania walioko kwenye maeneo yaliko machimbo hayo na sisi tunaoishi mbali na maeneo hayo.
Kwa maneno mengine ni ujinga kukata tamaa kwamba kitu kilichoko katika ardhi yetu sisi wenyewe Watanzania hakiwezi kututoa kwenye umaskini wetu, lakini eti kinaweza kwenda kuwapa utajiri wawekezaji waliowekwa na viongozi wasiowatakia mema wananchi wa nchi hii utajiri mara mia au elfu katika kipindi cha miaka michache tu. Na kwamba pamoja na kuishi katika umasikini kwa zaidi ya miaka 50 kabla ya uchimbaji madini, tunaweza tena kwa roho mbaya na ubinafsi wa viongozi wetu kuendelea kuishi kwa miaka zaidi ya 50 kama sio 100 kama masikini wa kutupwa katika nchi yetu.
Ipo bado nafasi ya Watanzania kuwawajibisha viongozi wao na wale waliokula na kufaidika na uwekezaji wa wale wanaochma madini na mafuta nchini mwetu leo. Na sio kunufaika tu, bali hata kutajirika na wale waliohamishwa katika maeneo yanakochimbwa madini na mafuta kuwa na hisa katika makampuni yanayofanya shughuli hizo katika maeneo yao ya kuzaliwa ambayo leo wamefukuzwa na kujikuta hawana tena makwao.
Huu ni wakati mzuri sana wa kutumia mchakato wa katiba mpya kuijulisha bila uoga wala kificho serikali kwamba mali asili na
madini ni ya wakazi wa eneo, tarafa, wilaya na mkoa husika, kwanza kabla ya yote ni mali ya wakazi hao na sio mali ya serikali wala chama chochote cha kisiasa hapa nchini. Sio haki na ni dhuluma iliyopitukia mipaka kwa kiongozi yeyote aliyeko Dodoma au Dar es salaam au popote pale alipo kunufaika na madini ya Bulyanhulu, Merelani, Geita, North Mara na kwingineko wakati mkazi na mzawa wa eneo husika anahukumiwa kulalia utajiri na kuamkia ukata na kufa masikini baada ya kufagiwa toka eneo husika.
Endapo kuna wanasiasa au viongozi yeyote walionufaika kwa kutoa kibali cha umilikaji eneo, uchimbaji na uuzaji madini nje wanastahili kujiwajibisha wao wenyewe kabla hawajawajibishwa na nguvu ya umma.
Tulivyozoea huko nyuma, eti, serikali ilijichukulia kama baba na mama wa Watanzania wote. Na mali yote ya umma ilikuwa ni mali ya serikali. Hivi leo mambo sivyo yalivyo. Kuna kikundi cha watu wachache wanaojifanya wao ndio wanaomiliki mali zote za Watanzania sio kwa kuzitunza kwa faida ya Watanzania wote bali kwa kuzitumia na kuzifuja kwa manufaa yao wenyewe.
Katika hali kama hii, katiba mpya, pamoja na mambo mengine lazima ieleze kinagaubaga kwamba ipo haja ya kutathmini upya mali asili, madini, mafuta na rasilimali nyingine upya na thamani hiyo iwe ni mtaji na mali ya wananchi wa eneo husika na siyo ya kundi la wajanja wachache ndani au nje ya serikali kwa niaba ya wnaasiasa na viongozi fulani.
Laiti ardhi na mali asili kwenye maeneo yanakochimbwa madini na vitu vingine vya thamani leo ingefanyika kwa haki na usahihi hakuna mkazi wa maeneo hayo leo angelikuwa ni maskini na baadhi yao wangelikuw ana hisa nono katika makampuni yaliyopo hivi leo. Ujinga, uoga na kutokujua kwa wanavijiji haki zao kumechangia hili. Na ndio maana baadhi yetu tuna kampeni za kutaka kuona madaraka zaidi kwa mikoa, wilaya, tarafa, kata na vijiji ili viongozi wa juu wa taifa wasitumie mianya iliyopo kunyonya na kuwadhulumu watu wa maeneo fulani nchini.
Hatua za mwanzo kufanyika
Makampuni yaliyopewa migodi sawa na bure yanatambua ukweli huu, kwamba yanatunyonya tena kwa ile mbaya sana. Na baadhi yao wameanza kuzinduka na kuanza kuwagawia Watanzania kama mababu zao walivyofanya huko nyuma, shanga, vioo, nyembe na vipande vya nguo ili sisi kwa ujinga wetu tuendelee kuwaachia kuokota almasi na dhahabu yetu sisi tukiona hicho wanachotudanganya nacho kwamba eti kina thamani. Ninaamini Watanzania wa leo, hata wale wasiokwenda shule, sio wajinga kiasi hicho. Watanzania hawawezi kabisa kudanganyika kwa barabara, maji, shule na vitu kama hivyo ambavyo serikali yao kutokana na kodi wanayotoa na kama viongozi wangelipunguza mishahara na posho zao kwa asilimi hamsini tu wangelivipata.
Wanavijiji wawatafute watoto wao waliosoma sheria, jeolojia na menejimenti kuja kusimamia vuguvugu la kudai haki ya asili na kutajirika na madini na maliasili katika eneo lao.
Kikundi cha kuelimisha, kuelewesha na kuhamasisha kudai haki na utajiri kiandaliwe mapema iwezakanavyo na kazi yake kubwa ikiwa ni kuwafanya wanajamii wote kuwa kitu kimoja katika madai yao ya kutajirika kutokana na madini au maliasili zao na sio mgeni au wageni tu kunufaika na mali zetu, wakati wao tayari ni matajiri wa kutupwa, eti tu kwa kuwa kuna viongozi na wanasiasa wetu fulani, wananufaika na uwekezaji huo. Kitu kama hiki kinaendana kinyume kabisa na maadili aliyotuachia baba wa taifa pamoja na katiba yetu hii chakavu tuliyonayo leo.
Ni vizuri pia kwa viongozi wa jamii kusaidiwa na vyama visivyo vya kiserikali kwenda kwenye nchi ambazo tayari wananchi wake wananufaika na madini na mali asili zao mbalimbali kama vile Argentina, Bolivia, Peru na kwingineko.
Baada ya watu kueleweshwa na kuelimishwa kwamba wana nafasi bado ya kuwa matajiri na kuwa na hisa katika makampuni ya migodi kitakachofuatia
ni kampeni ya nyumba kwa nyumba ili kuhakikisha kwamba kila mpenda mabadiliko na maendeleo anakuwa ni sehemu ya vuguvugu na kila mtu kukubali kwanza kula shubiri kabla asali haijapatikana.
Baada ya kila nyuma na wakazi wake kulielewa na kulikubali hili kazi inayofuatia ni kuwa na mikutano ya mtaa, kata, tarafa, wilaya na mkoa ifanyike ili kuwafahamisha viongozi sababu, malengo na madhumuni ya vuguvugu la kurejeshewa haki na utajiri wa maeneo ya wazawa yaliyoachiwa wawekezaji kimakosa au kiujanja na baadhi ya wanasiasa na viongozi nchini.
Zoezi hili litapima viongozi mbalimbali kama wanasimama kuwatetea wananchi na maslahi yao au viongozi hao ni vibarakala wa serikali na vyama vya kisiasa na hawana habari kabisa sio tu na kesho ya wananchi husika bali hata leo yao pia hawana habari nayo.
-mikutano ya kuelimisha uongozi wa taifa
Hii ina maana mbunge, mkuu wa wilaya, mkuu wa mkoa ni lazima asimame na kuhesabiwa. Hesabu hii ndiyo itakayoamua kama nchi inafaa kuwa na viongozi wa kuteuliwa au wa kuchaguiwa na wananchi wa eneo husika. Maana unaweza kukuta wananchi sio tu wananyonywa mali asili na rasilimali zao nyingine na serikali kuu na viongozi wake, lakini pia wanabebeshwa mizigo wasiyostahili kubeba.
Masharti muhimu:
Ili kazi hii ya kudai haki na utajiri tokana na maliasili za wananchi ifanikiwe yapo masharti kadhaa:
Kwanza, zoezi zima lazima liendeshwe kwa nguvu za umma chini ya usimamizi ya watoto na wajukuu wa jamii husika waliosomea masuala ya sheria, madini, siasa na utawala, menejimenti, sayansi ya maamuzi, teknohama, fedha na uwekezaji na kadhalika.
Thamani ya mapato kutokana na uchimbaji dhahabu ifanyike kulingana na mapato yatakayopatikana tokana na uchimbaji na uuzaji dhahabu toka mgodi uanzwe kuchimbwa hadi dhahabu kumalizika kuchimbwa. Hii ina maana kama dhahabu imeanza kuchimbwa mwaka 1997 na itamalizika 2047, hii ni sawa na mapato ya miaka 50 na hesabu hii ndiyo itakayogawanywa kuwalipa fidia wanavijiji husika kama wabia pamoja na mwekezaji, serikali kuu, serikali ya mkoa, serikali ya wilya na wanaharakati watakaochangia kufanikisha jambo hili.
Ni lazima baada ya hpo kugawana faida sawa na wawekezaji katika uchimbaji dhahabu na madini kama hayo, na pale kampuni inaposhaurika ni vyema zaidi wananchi wa eneo husika na sio viongozi wasiohusika na eneo hilo kupewa hisa katika kampuni inayoshughulika na uchimbaji wa madini husika.
Uchimbaji dhahabu usilete madhara kwa wanadamu au mifugo, na kampuni au mtu yeyote anayesababisha madhara au vifo vya binadamu au wanayma kutokana na uchimbaji wa madini laima ahukumiwe kwa mujibu wa sheria za mauaji zilizopo hivi sasa.
Ni lazima wanavijiji ambao maeneo yao yalikwishataifishwa na kubinafsishiwa wawekezaji, walipwe fedha wanayostahili na kama fedha hiyo ililiwa na wakubwa basi irudishwe au mwekezaji alipe upya wanavijiji.
Wanasheria wanaojitolea kwa gharama ndogo wasimamie zoezi zima la ulipwaji upya wanavijiji. Wanasheria hawa wachangie pia kupatikana wawekezaji mbadala kutoka Brazili, Uchina, Vietnam, Korea, India, Urussi na kwingineko kule ambako kutawapatia wananchi wawekezaji watakaowanufaisha na kuwatajirisha wao pia kuliko wawekezaji hawa wa kutoka Kanada, Marekani na Afrika kusini waliopo hivi leo na wanaosadikiwa kula na kulindwa na wale walioko madarakani.
Wanavijiji wapewe hisa katika migodi au kampuni za dhahabu na madini mengine kwenye maeneo yote ambako migodi imeanzishwa na wao ndiko kulikokuwa na makazi yao ya awali toka walipozaliwa hadi kuhamishwa kwa mabavu na bila fidia au kwa kulipwa fidia sawa na mzaha!
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment