Sunday, February 6, 2011

Mfumo upi wa kiuchumi na kisiasa Tanzania

KARNE ya ishirini ilishuhudia mataifa duniani yakikigawanyika na aghalabu tofauti zao zimetokana na mifumo tofauti ya uchumi kila nchi iliyoamua kufuata.

Toka ukomunisti au ujamaa uliposambaratika huko Urusi na Ulaya ya Mashariki kuna wanaodhani kuwa tofauti hizi zimefikia kikomo.

Lakini tunaweza kufanya makosa tukifanya hivyo. Ikumbukwe kuwa katika miaka ya 1930 wengi waliamini kuwa ubepari umefeli na palihitajika mfumo mwingine wa kiuchumi.

Waliofikiri hivyo waliumbuliwa. Baada ya miaka michache tu ubepari ulirudi na nguvu mpya ingawa ulitofautiana kwa kiasi kikubwa na ule ubepari uliotangalia.

Ubepari umevuka mitihani kadhaa kwa ushindi mkubwa. Lakini leo tena ubepari unakutana na mitihani mingine.

Kuna wanaoamini kuwa mfuko
wa soko huria, himaya za kitaifa na dini hivi leo zinashindwa kukubaliana na matatizo yaliyoko mbele yake.

Matatizo hayo ni pamoja na umasikini, maradhi, ujinga na vita kati ya nchi na nchi na vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Mwaka 1997 ilionekana kwa wengi kuwa ujamaa umeshindwa lakini kama watu wa 1930 walivyofanya makosa kusema kuwa ubepari umeshindwa dalili zimeanza kujitokeza kuwa hilo nalo pia ni kosa.

Kufikia mwaka 2002 ilikuwa ni dhahiri kuwa nchi iliyobebea katika siasa ya ubepari-Marekani na mama yake Uingereza ina matatizo kutokana na mfumo wake wa kibepari.

Kwa bahati mbaya viongozi wa sasa wa Marekani na Uingereza wanaamini kuwa matatizo hayako ndani kwao bali yako nje. Kwa hivyo wameanza kusaka wachawi wao nje, kwanza alikuwa Osama, kisha Iraq, kesho Iran, Korea Kaskazini na keshokutwa sijuia atakuwa nani.

Lakini kinachoonekana ni kuwa ubepari kwa kutegemea mno unyonyaji hauwezi kupona bila kuwepo watu na mataifa ya kunyonya.

Hii ndio sababu iliyoifanya Uingereza na Ufaransa kuwafanya wengine watumwa wao kupitia ukoloni mkongwe.

Na ni sababu kama hiyo pia iliyowafanya Wamarekani kuwatawala Amerika Kusini na pale Wananchi wa nchi husika walipokataa kutawaliwa basi nchi hizi za kibepari zilizua zahama za kila aina ili tu kuonyesha kuwa wengine hawawezi kujitawala ila ni wao tu wanaojua kujitawala.

Leo Marekani ya Kusini imeanza kuamka tena. Inauliza kwanini mambo yao yasimamiwe na Marekani.

Marekani imeanza kuanja mbali. Na ni Afrika tu ambayo haijafikwa bado na nuksi ya kuwepo kwa Wamarekani ndani yake (ingawa huko Angola na Kongo) walikwishaonjwa kidogo.

Damu iliyomwagika Marekani Kusini na kati kwa kiasi kikubwa inalia na Wamarekani.

Nchi hiyo ilipojiingiza pia Mashariki ya mbali ndio mabalaa yakaanza huko, kumbuka China, Korea, Vietnam, Ufilipino na kwingineko.

Hivi sasa nchi hiyo kwa kuruhusiwa na nchi za Kiarabu na baadhi ya nchi za Kiafrika kuweka makambi ya kijeshi katika nchi hizo na kuanza kuwakoroga Waarabu na Waafrika kisiasa na kiuchumi wengi wanaamini mikosi ya Vietnam na Marekani ya Kusini sasa inahamia katika nchi za Kiarabu na Kiafrika.

Ni wajibu wa dunia kuielimisha Marekani kuwa siasa zake za kibabe na unyonyaji wake uliokithiri utaifikisha dunia pabaya. Hakuna mtu au nchi inayoweza kuishi kwa kukopa au kutegemea jasho na rasilimali za wengine. Lakini hiki ndicho hasa kinachofanywa na mabepari.

Katika hali kama hii ambayo kama hadithi ya Mbweha na Mwanakondoo mabepari huwasingizia hata watoto kuwa ndio wanaochafua maji yanayotiririka tokea kule wao waliko ni vema kujiuliza kama kweli ubepari ndio mfumo wa siku zijazo?

Kweli mfumo wa Kisovieti au wa kijamaa ulikuwa na matatizo yake. Lakini tumekaa na kujiuliza matatizo hayao yalikuwa nini?

Mjadala kuhusu mfumo upi wa kiuchumi na kisiasa ambao nchi kama yetu unatakiwa kuufuata ili tuwe na jamii na utawala bora sio mjadala wa kuukwepa. Na viongozi wa kweli katika jamii yaani wafanyabiashara na wazalishaji mali wengine wanstahili kubeba gharama za kuona mjadala huu juu ya hatima ya nchi na siasa zake unafanyika mara kwa mara.

Mijadala kuhusu mfumo upi wa kiuchumi na kisiasa unafaa kufuatwa aghalabu huegemezwa juu ya mifumo mbalimbali iliyopo na kujaribu kuanisha na kuchagua kipi kinachofaa ili kuijenga jamii husika bila kuwepo migogoro inayoweza kuisambaratisha jamii husika.

Katika kufanya uchambuzi wa mifumo ya kiuchumi na kisiasa ni vyema kuanza kwa kufafanua ni kipi kilicho bora na jamii inachostahili kuwa kwa kufanya hivyo tunaweza kujifunza mengi ikiwa ni pamoja na kwanini mifumo yta kiuchumi na kisiasa wakati mwingine hushindwa kuzaa matunda yanayotegemewa.

Wanauchumi wanabainisha kuwa mifumo bora kama ilivyochaguliwa na watu mbalimbali duniani ni pamoja na ule wa soko huria (ybepari mkongwe); ubepari unaodhibitiwa na serikali; uchumi unaosimamiwa na serikali (serikali kushika hatamu); ujamaa unaoruhusu soko huru na mfumo unaoruhusu wafanyakazi kusimamia maisha na kazi zao katika jamii husika.


Ni dhahiri kuwa kila mfumo wa uchumi duniani umeshawahi kuijaribu mifumo mingine wakati fulani na matokeo yamehitilafiana kutoka nchi moja kwenda nyingine.


Ubepari mkongwe ni mfumo wa kiuchumi kama unaofuatwa na Marekani au Uingereza. Nao huwaachia watu kazi zote za uzalishaji mali na serikali huwajibika zaidi katika suala la kukusanya kodi, kutoa huduma muhimu kwa jamii kama ulinzi, ujasusi, usalama na utunzaji mazingira.

Yaani serikali hukifanya kile ambacho watu wakipewa wataumiza watu wengine au kile ambacho watu hawapendi kukifanya kwa sababu hakina faida wala tijara.

Ubepari unaosimamiwa na serikali ni mfumo unaofanana kwa kiasi kikubwa na ubepari mkongwe lakini hapa ni kuwa serikali ina ruksa ya kufanya maamuzi fulani yanayoingilia jinsi kipato kinavyopatikana na kutumika miongoni mwa Wananchi wake.

Hili hufanyika ili kupunguza makali ya ubepari katika unyonyaji na kujaribu kuleta usawa na haki fulani katika jamii kwa kutumia vyombo vya serikali.

Uchumi unaosimamiwa na seirkali sio tofauti na mfumo Tanzania uliokuwa ukifuata toka mwaka 1967 hadi Rais Mwinyi alipoingia madarakani na kuanza kuruhusu soko huria kwa kiasi fulani. Ingawa kabla yake Rais wa kwanza alisharuhusu ulegezaji masharti ya uchumi uliosimamiwa na serikali.

Uchumi wa kijamaa unaokubali soko huru kwa kiasi fulani ni mfumo unaojaribu kunufaika na mazuri ya ubepari katika uzalishaji mali na ukuzaji kipato cha jamii na taifa bila kuruhusu mabaya ya ubepari kutamalaki kila mahala katika jamii na hasa unyonyaji ulikokithiri na uvunjaji sheria wa hali ya juu.

Mifumo inayoruhusu wafanyakazi kuendesha uchumi inapatikana katika nchi ambazo vyama vya wafanyakazi vina sauti kubwa katika kuamua masuala yanayohsu uchumi na siasa za nchi. Ujerumani ina sifa hii kwa kiasi fulani ingawa kwa kiasi kikubwa ni nchi ya kibepari na kuna baadhi ya nchi kadhaa za Marekani ya Kusini na kati ambako vyama vya wafanyakazi vina mchango mkubwa katika maendeleo na amani ya nchi.

Hivi sasa kuna madai kuwa Tanzania haijui iko katika mfumo gani. Lakini wanasiasa na wanaitikadi (kama wapo) wa chama tawala na vyama vingine wameshindwa kuhamasisha majadiliano yoyote ya maana ili nchi ieleweke inatoka wapi na inakwenda wapi.

Pengine hili linatokana na ukweli kuwa ni wachache miongoni mwa wanasiasa hao wanaoelewa nadharia za uchumi muafaka kiasi cha kuzungumza kwa uhakika juu ya masula yanayohusu mifumo inayofaa kufuatwa na taifa.

Kama ndivyo, huu utakuwa mchango wangu mdogo katika kuwafungua watu macho juu ya mifumo iliyopo ili tuweze kuitafiti zaidi na kuanza kuizungumza ili tuweze kuelewashana na hatimaye kufikia muafaka kuwa Tanzania inastahili kujitmbulisha na mfumo upi.

Mfumo wa ujamaa uliwaunganisha Watanzania kwa kiasi kikubwa maana wote tulijatmbulisha nao. Kuna waliokuwa hawautaki lakini kutokana na wingi wa waliokubali ilibidi nao wajitambulishe nao hivyo hivyo ili kulinda maslahi yao ya kiuchumi na kisiasa.

Hivi sasa ni dhahiri kuwa wengi waliokuwa wajamaa jana leo ni mabepari na hawataki kabisa kusikia kitu chochote kuhusu ujamaa.

Lakini maskini hawa ni bendera fuata upepo na watu wanaotanguliza malshi yao binafsi mbele na sio maslahi ya walio wengi.

Swali linabakia pale pale kuwa ni mfumo upi wa kiuchumi na kijamii Tanzania na Watanzania kwa ujumla wao wanastahili kuuiga au kuufuata?

Ni ubepari mkongwe ili tuwe kama Marekani na Uingereza na matatizo yao ya ukubwa, kuishi kwa kunyonya nchi na watu wengine na wakikataa tuwafanyie vita?

Ni mfumo wa ubepari unaosimamiwa na serikali kama ule wa Ufaransa?

Au ni mfumo ule wa zamani kwenye enzi za hayati Nyerere wa serikali na chama kushika hatamu na kuwa na mameneja na viongozi wanaojiiita wajamaa kumbe wabinafsi wakubwa na mabepari walio likizoni?

Au ni mfumo kama ule wa China ambao chama tawala huko kimekubali kutumia mazuri yote ya ubepari katika kuujenga mfumo imara wa uchumi na misingi bora ya maendeleo ya kisayansi na kiteknolojia?

Lazima taifa lifikie mahala likae, lijadili na likubali na liutangazie umma juu ya uamuzi utakaofikiwa kuhusu ni mfumo gani wa uchumi na kijamii tutakuwa tunaufuata katika karne hii ya 22? Hatuwezi kuendelea kuwaacha Watanzania kwenye giza.

No comments:

Post a Comment