Sunday, February 6, 2011

Dalili za Chama Kinachosambaratika

CHAMA chochote cha kisiasa au shughuli nyingine kama ilivyo kwa kundi lolote la watu, liwe kubwa au dogo, likishakaa pamoja kwa muda mrefu na kuzoeana kupita kiasi huwa linapoteza sio tu dira au visheni yake bali pia hekima na busara zake katika kutathmini uhalisia wa mambo na maamuzi ya kimaadili au kiitikeli bali pia hata uwezo na kasi yake ya kufanya maamuzi kwa wakati unaotakikana na pale yanapofanyika haraka haraka, maamuzi hayo yanakuwa hayana ubora unaokubalika.

Chama kinachoathirika na gonjwa la 'ndivyotunavyofikiri' (groupthink) kama ulivyogunduliwa na kuelezewa na guru wa menejimenti ya makundi ya watu, Prof. Irving Janis, sikuzote hudharau njia na fursa mbadala na hujikuta kikifanya maamuzi bomu na yaliyo na sura ya kuvifanya vyama vingine vya kisiaasa na makundi mengine ya watu kuonekana ni ya vichaa, watu hatari na wasiojua watakacho.

Chama au kundi lolote linaweza kuugua ugonjwa wa 'ndivyotunavyofikiri' hasa pale wanaounda chama hicho au kundi hilo wametoka kwenye hali au mazingira yanayofanana na wamefinyangwafinyangwa au wote kulazimisha kuwa na mtazamo au msimamo mmoja pamoja na kufikiri sawasawa kama maroboti.

Ugonjwa huu pia huwaathiri kwa kiasi kikubwa wale wanaoziba masikio na macho yao kuona yanayotokea nje ya chama au kundi lao na wale wasiosikia mawazo au fikra mpya au tofauti toka nje ya chama au kundi husika. Au kwa kifupi wale wote wanaoshindwa kuzisoma na kuzielewa alama za mabadiliko ya nyakati zinazoanza kusheheni kila eneo la kijamii, kisiasa na kiuchumi.

Aidha, kutokuwepo kwa kanuni na taratibu zinazoeleweka za kufikia maamuzi makubwa yanayohusu chama au kundi na watu wengine nako pia huchangia kupata gonjwa hili la 'ndivyotunavyofikiri'.

Ni rahisi kujua kama chama au kundi linaugua ugonjwa wa 'ndivyotunavyofikiri' kwa sababu Javis ameelezea kuwepo kwa dalili kubwa kama nane hivi. Dalili hizo ni hizi zifuatazo:

• Kujidanganya kuwa hakuna kisichoweza kufanyika na sio rahisi kushindwa na chama au kundi lingine la watu. Hili hujenga kujiamini kupita kiasi kwa viongozi na wafuasi wa chama, jambo ambalo husababisha viongozi na wafuasi hao kufanya majaribio na mambo ya hatari yanayoweza kukigharimu chama na wanachama wake na pengine hata nchi husika;

• Kuhalalisha kwa pamoja kiurahisi bila ya kuhoji uamuzi wowote unaofanywa na chama au kundi. Wanachama huwa hawasikii la muazini au la mchota maji na hudharau maonyo yote wanayopewa na huwa wagumu kubadili mitazamo na misimamo yao juu ya mambo mbalimbali;


• Kudhani wao ni wacha-Mungu, watakatifu na wenye haki zaidi kuliko wengine. Wanachama huamini katika imani na uhalali wa imani au msimamo wao na hivyo hudharau haki na itikeli za mtazamo na msimamo wao wakati wa kufanya maamuzi au jambo lolote linalohusu jamii au jumuiya nzima;

• Hudhihaki vyama au makundi mengine katika jamii. Hisia za sisi ni kitu kimoja au huyu ni mwenzetu na wale ni maadui zetu hutawala na hivyo kusababisha kukosekana kwa matumizi yoyote ya akili, busara na hekima katika kushughulikia migogoro kwa njia sahihi na mujarabu;

• Shinikizo kwa wanaohitilafiana na msimamo wa viongozi wa chama au kundi husika. Wanachama wote, wakiri au wasikiri hivyo, huwa wanapata shinikizo kubwa toka kwa wenzao kutotofautiana kabisa na misimamo na mitazamo ya chama au kundi husika;

• Kujichuja wenyewe. Mashaka ambayo baadhi ya wanachama wanayo juu ya uamuzi au jambo lolote juu ya msimamo wa pamoja uliofikiwa (mathalani, kuilipa Dowans) huwa havipewi fursa na ni adimu kutokeza hadharani.

• Kujidanganya kuhusu juu ya wote kukubaliana jambo kwa pamoja. Fikra, misimamo, mitazamo na uamuzi wa wengi huchukuliwa kwamba ni watu wote kwa pamoja wamekubaliana ingawama mara nyingi ukweli huwa ni kinyume kabisa na hilo. Hakukosekani wanaolikataa wazo au jambo bali hata wakiwa wengi maji hufuata mkondo kwa kwenda na msimamo wa viongozi na wapiga debe wa chama au kundi husika.

Walinzi wa mawazo na fikra wanaojichagua na kujipandikiza wenyewe ili viongozi wasipate habari mbaya au habari viongozi wasizotaka kusikia au ambazo wakisikia watafanya maamuzi tofauti kabisa na yale wanaowazunguka wanayoyataka. Watu wachache hujichukulia wenyewe jukumu la kumlinda kiongozi na wafuasi wake dhidi ya habari zozote mbaya au zinazotoa picha tofauti kabisa na ukweli ulivyo kama unavyoelezwa na habari za kupikwa na kuletwa mezani makusudi kutoa picha ya uongo na kweli kuhusu uamuzi au hali halisi ilivyo. Habari zozote zenye harufu mbaya au picha chafu huchujwa na hazifiki mbali. Hili hufanywa pia kwa kutumia vyombo vya habari vinavyomilikiwa na chama na serikali husika.

Ndivyotunavyofikiri hutokea pale chama au kundi linapokuwa na umoja unaolazimishwa na panahitajika pafanyike maamuzi makubwa ya kichama, kiserikali au kitaifa. Maamuzi yenyewe yakihusu aghalabu riziki na uhai wa chama na viongozi wake pia. Hili hulazimisha viongozi kukubalina penda usipende juu ya jambo husika; hakuna anayekuwa na motisha ya kulichambua na kulipangua jambo na kulipanga upya ili kupata uamuzi sahihi; na hudharau au kupuuza maamuzi mbadala mengi ambayo huwa hata hayafikiriwi kabisa hata kama muda unaruhusu.

Shinikizo hili husababisha suala la ubora wa maamuzi kutozingatiwa kabisa na uhai na umoja wa chama na viongozi wake kupewa kipaumbele zaidi kuliko kitu kingine. Agjhalabu uamuzi huwa ni bora wote tufe, kuliko tu chama na wanachama wake kufa (kisiasa).

Maamuzi yanayofanywa wakati chama au kundi linaugua 'ndivyotunavyofikiri' huwa hayana uwezekano wa kufanikisha jambo lililokusudiwa hata kidogo.

Katika nchi kama hizi zetu za Kiafrika kutokana na heshima ya ’ubaba wa kitaifa’ na ’ukombozi au uhuru wa bendera’ wale walioshiriki katika harakati za uhuru huwa wanaheshimiwa mno na kubakizwa madarakani muongo baada ya muongo. Lakini sasa subira imeanza kupungua kwa vijana wetu. Wanashindwa kuvumilia kuwa chini ya rais huyo huyo toka wakiwa chekechea, msingi, sekondari, vyuo vikuu hadi wanakuwa joblesi na ’unwanted and unloved’ nchini mwao na bado mtu anang’ang’ania kubaki madarakani.

Pamoja na hili ni kichekecho kuona wale wanaopewa madaraka ya kuwa viongozi wa vyama vikongwe Afrika wanakuwa ni wachekeshaji, wasanii na wababishaji na sio watu siriazi na kile wanachokifanya na wala huwa hawajui wapi dunia inakoelekea.
Aidha, .Viongozi huendelea kukanusha kuwa chama au kikundi hakina tatizo, mgawanyiko wala misiguano hata pale kinapokuwa kinachungulia kaburini;

. Viongozi huwa wanajishughulisha na mambo ambayo yangefanywa vizuri zaidi na watu wa chini, huku wakiacha kufanya yale yanayowahusu wao na hivyo kutumia muda na rasilimali kwa vitu visivyo na faida kwa chama au kikundi husika;

. Hujitahidi kufanya sherehe, mbwembwe na kujionesha kwa kila aina ili kwa nje kionekane kwamba ni chama au kikundi chenye umoja na bado chenye nguvu na uwezo wa kufanya mambo ya maana na kumbe sivyo;

. Huonesha upendeleo wa wazi kwa wake/waume zao, watoto wao, ndugu zao, jamaa zao , marafiki wao na wale wote wanaonufaika kwa njia moja au nyingine kutokana nao;

. Huwa hakijali kabisa muda unavyoyoyoma na kupotea na huamini hakuna anayeweza kukiharakisha kwa hili au line na hakuna sababu ya kuharakisha kitu kwa kuwa kiko madarakani;

Iko mifano mingi ya 'ndivyotunavyofikiri' toka sehemu mbalimbali duniani. Mathalani, mojawapo maarufu ni lile la serikali ya Marekani kushindwa kutabiri kushambuliwa kwa nchi hiyo na Japani zaidi ya mika 60 iliyopita; Uvamizi wa Marekani huko Cuba ulioshindwa vibaya; na vita vya Marekani dhidi ya Vietnam kaskazini isiikomboe Vietnam Kusini.

Hivi karibuni, tumeona matukio ya Blair na Bush, kuziingiza Uingereza na Marekani katika vita dhidi ya Iraq kwa sababu ambazo hazikuwa za kweli na matokeo ya maamuzi hayo kwa nchi hizo na dunia kwa ujumla.

Aidha, jinsi Waafrika walivyolazimishwa na nchi hizo za Uingereza na Marekani kukubali kujiunga na vita dhidi ya ugaidi na fedha chafu bila ya watu wa nchi husika kuachiwa kutoa maoni na misimamo yao juu ya jambo hilo. Matokeo yake yakiwa kupandwa mbegu za chuki dhidi ya Uislamu na Ukiristo Afrika na kwingineko.

Tumeona 'ndivyotunavyofikiri' pia ikiathiri Umoja wa Afrika (AU) kuhusiana na Al Bashir wa Sudan; Mugabe wa Zimbabwe; wachocheaji mauaji ya Rwanda na Kenya na sasa Cote d'Ivoire. Kote huku kwa kiasi kikubwa maslahi ya wasionacho hayakuzingatiwa ila yale ya wale walichonacho tu. Wakubwa wanatambua fika ridhaa yao kwa jambo kama hilo ni kaburi na mauti yao pia kisiasa na hususan kwa madikteta uchwara wanaopora mamlaka ya wananchi katika tawala zao.

Huko nyuma kiasi, wakati Watanzania wakidanganywa na kudhulumiwa na siasa za chama kimoja maamuzi kadhaa yaliyofanyika huko wahusika wakiugua 'ndivyotunavyofikiri' ni pamoja na Azimio la Arusha, Ujamaa na Kujitegemea, kuua serikali za mitaa, uanzishaji wa vijiji vya ujamaa, kuua vyama vya ushirika, kuua michezo mashuleni, kuua matumizi ya lugha za kikabila katika magazeti na redio, uamuzi wa kuhamia Dodoma na maamuzi mengine mengi kama hayo yote yaliathirika si haba na gonjwa la ndivyotunavyofikiri na ziada yake ndivyotunavyokubaliana.

Kiujumla kutokana na uoga na kutokujua nafasi yao kama mhimili pekee katika mihimili iliyopo unaoweza kupiga vita rushwa, wizi wa kura, ufisadi na kuwa na watu waovu kama viongozi vyombo vyetu vya habari na hususan televisheni na redio vimewaangusha Watanzania, na kwa bahati mbaya ni Watanzania wenyewe walioliruhusu hili kutokea.

Hususan, wale ambao kabla ya kuwa viongozi walivienzi vyombo vya habari lakini baada ya kupewa uongozi sasa wanataka kuvigandamiza vyombo vya habari kama sio kuviulia mbali.


Chama si mtu mmoja. Mtu mmoja hufa na husahaulika baada ya muda si mrefu. Chama ni kundi la watu. Kundi ambalo kama likiweza kujizaa upya kila inapohitajika huweza kuishi milele. Kinachotakiwa kwa chama chochote kinachoona kuwa kinaugua gonjwa hili kukaa na wataalamu wa masuala haya na kuanza kukisuka chama upya ili kukabili zama mpya. Na wakati ni huu, hakuna kabisa muda wa kuchelewa.

No comments:

Post a Comment