Ukitanguliza mwili,
Nyuma ifate akili,
Hupati pendo la kweli,
Na roho hugawanyika!
Siukimbilii mwili,
Najua wake muhali,
Umkutapo baradhuli,
Pendo sumu hugeuka.
Naitafuta akili,
Tena kwa hali na mali,
Sio kwayo taamuli,
Bali kwayo tajamali.
Naitafuta kauli,
Murua tena sahili,
Itoayo afadhali,
Mashaka yanaponifika.
Nazitafuta dalili,
Za bashasha na adili,
Na pendo bila ubahili,
Nikatakwa, nikataka.
Nazitafuta amali,
Za majibu na maswali,
Kuzijenga zetu hali,
Toka chini, juu tukafika.
Naitafuta asali,
Toka nyuki wa asili,
Na sio ile ya kunakili,
Nilambe na kutosheka!
Sitaki nafuu ghali,
Nikajabwagwa chali,
Bila kisomo cha Laili,
Nyota njema ikishuka.
Sitaki cha bilkuli,
Ima fa ima kivuli,
Cha mshaka ya samli,
Kupika kisichopikika.
Sitaki kiwiliwili,
Nataka yako akili,
Inifanye mie kamili,
Kiroho pia kimwili!
Tuesday, June 30, 2009
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment