Linasifiwa waridi, tena sana duniani,
Nani hili kulikaidi, asiyelisifu nani?
Ni wachache kwa idadi,waridi wasothamini,
Mfano mie kusifu, harufu ya Jasmini.
Kulienzi sina budi,waridi rangize shani,
Hautimii mradi, kutosifu Jasmini,
Kwalo mimi shahidi, kwa macho na moyoni,
Nd'o kisa mie kusifu, ua lake Jasmini!
Ua hili maridadi, kalijalia Manani,
Linatia ubaridi, joto ukilibaini,
Na lapandisha mdadi, baridi ikikuhaini,
Hakika yanipendeza, harufu ya Jasmini.
Sio wengi hulifaidi, linapenda faraghani,
Mchana katu abadi, harufuye huioni,
Ila usiku taradadi, nje, uani na chumbani,
Utaisikia kokoe, harufu ya Jasmini.
Chumbani bure waridi, ni ndogo yake thamani,
Kitandani hufaidi, ila uwe na Jasmini,
Huba huwa kama Iddi, sikuzote u rahani,
Usingizi laini kwa harufu ya Jasmini!
Tuesday, June 30, 2009
Subscribe to:
Post Comments (Atom)

No comments:
Post a Comment